Baraza la Mawaziri lapitisha bajeti uchaguzi wa marudio

Katibu wa Baraza la Mawaziri Henry Rotich

Muktasari:

Kiasi hicho cha fedha ni pungufu kwa Sh2 bilioni hasa ikizingatiwa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) ilikuwa imeomba Sh12.2 bilioni kwa ajili ya shughuli za uchaguzi wa marudio baada ya ule wa kwanza uliompa ushindi Rais Uhuru Kenyatta kufutwa na Mahakama ya Juu mapema mwezi huu.

Nairobi, Kenya. Baraza la Mawaziri, katika kikao chake kilichofanyika Alhamisi ikulu chini ya mwenyekiti wake Rais Uhuru Kenyatta lilipitisha bajeti ya Sh10 bilioni kwa ajili ya maandalizi ya uchaguzi wa marudio wa rais uliopangwa Oktoba 26.

Kiasi hicho cha fedha ni pungufu kwa Sh2 bilioni hasa ikizingatiwa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) ilikuwa imeomba Sh12.2 bilioni kwa ajili ya shughuli za uchaguzi wa marudio baada ya ule wa kwanza uliompa ushindi Rais Uhuru Kenyatta kufutwa na Mahakama ya Juu mapema mwezi huu.

"Baraza la Mawaziri leo (juzi) limeidhinisha kutolewa Sh10 bilioni ili kugharimia uchaguzi wa marudio kwa kura ya urais. Kiasi hicho kimetolewa kwa kuzingatia mapendekezo ya bajeti iliyowasilishwa na IEBC," imesema taarifa ya msemaji wa ikulu Manoah Esipisu.

Awali Katibu wa Baraza la Mawaziri Henry Rotich alikadiria kwamba uchaguzi wa marudio unaweza kugharimu zaidi ya Sh15 bilioni ikiwa 'shughuli zinazohusu kwa upana usalama zitaingizwa'.