Profesa Kabudi aeleza walichokubaliana na Barrick

Muktasari:

  • Katika makubaliano hayo Serikali na Barrick watakuwa wakigawana asilimia 50 kwa 50 ya faida

Dar es Salaam. Waziri wa Katiba na Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi amesema kuwa kampuni ya Barrick imekubali masharti yote ya sheria mpya madini mazungumzo yao.

Profesa Kabudi amesema hayo leo Alhamisi wakati akitoa taarifa kwa Rais John Magufuli kuhusu majadiliano kati ya Serikali na kampuni ya Barrick.

“Pia wamekubali Serikali kuwa na asilimia 16 kwenye migodi yote ya Barrick na kwamba kwenye mgawanyo itakuwa ni asilimia 50 kwa 50.

Amesema mbali na hilo pia mapato yote ya kampuni hiyo yatawekwa kwenye akaunti zilizopo hapa nchini na kwamba makao makuu yao yajengwe Mwanza.

Amesema mbali na hilo pia kampuni hiyo imekubali kuwa kila kampuni inayoendesha migodi kuachana na wafanyakazi wa mikataba bali waajiriwe wazawa na wasiwe wanakaa kambini.

“Hii ni kuachana na mtindo wa sasa wa kuwaweka watu wazima kwenye makambi,”amesema Profesa kabudi.

Awali Mwenyekiti Mtendaji wa Barrick, John Thonton amesema makubaliano hayo yataenda kuidhinishwa na Bodi nchini Uingereza ambayo ina hisa asilimia 64.

Amesema wamekubaliana pande hizo mbili watakuwa wanagawana faida asilimia 50 kwa 50 kama alivyosema Profesa Kabudi.