Bashe: Kupeleka hoja binafsi ni wajibu wangu kikatiba -VIDEO

Mbunge wa Nzega Mjini (CCM),Hussein Bashe

Muktasari:

Bashe amesema amefanya utafiti wa matukio hayo kwa kipindi cha miaka mitano. 

Dar es Salaam. Mbunge wa Nzega Mjini (CCM),Hussein Bashe amesema amechukua hatua ya kuwasilisha hoja binafsi kwa Katibu wa Bunge kwa kuwa ni wajibu wake kikatiba.

Bashe amesema amechukua hatua hiyo kwa sababu amefanya uchunguzi kwa miezi mitano juu ya matukio ya utekaji, mauaji na watu kupotea yaliyotokea tangu mwaka 2010.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Machi 8, 2018 huku akinukuu vifungu vya Katiba,  Bashe amesema hoja yake hiyo inawakilisha mawazo ya wananchi kuhusu matukio ya uhalifu, utekaji na watu kupokea. 

Amesema katika hoja hiyo, ataambatanisha matukio ya tangu mwaka 2010 yakiwamo yaliyotokea katika uchaguzi mbalimbali kwa maelezo kuwa amefanya uchunguzi wa kutosha. 

"Watanzania wanalalamika na haya ninayoyafanya yapo katika Katiba ya chama changu. Msingi wangu wa kubeba hii hoja ni katiba ya chama changu na katiba ya nchi.  

"Ili CCM iendelee kuimarika lazima isimamie misingi yake. Nakwenda bungeni na hoja hii kama mbunge wa CCM. Nimechukua hatua hii sababu ni kiapo changu kwa Chama Cha Mapinduzi. Siwezi kulalamika mitaani nitatumia nafasi yangu kuwasilisha jambo hili," amesema.

Amesema mpaka sasa viongozi wa CCM waliouawa Kibiti wanafika 14, huku viongozi wengine wa upinzani nao wakipoteza maisha akiwamo aliyekuwa kiongozi wa Chadema, Alphonce Mawazo. 

"Nani anafanya haya matukio mbona hakuna haki? Rais amezungumzia mambo haya likiwamo la Akwilina. Ila kauli ya Rais haizuii sisi wengine kufanya haya nifanyayo. Azory Gwanda mpaka leo hajulikani alipo," amesema. 

Amesema kuwasilisha hoja hiyo ni kutimiza wajibu wake kama mbunge wa CCM,

"Nitaheshimu mawazo ya wengine kuhusu hoja yangu ili mwisho wa siku tufikie uamuzi kwa maslahi ya nchi na chama change,” amsema.

Amesema amefanya utafiti kwa zaidi ya miezi mitano na kwamba ataukabidhi utafiti huo ili kila Mtanzania ajue mambo hayo aliyoainisha katika hoja yake.