Bavicha wahoji Lowassa kwenda kwa Rais Magufuli

Muktasari:

Imesema Lowassa hawezi kumpongeza Rais Magufuli wakati vyama vya siasa vimezuiwa kufanya mikutano

Dar es Salaam. Baraza la Vijana la Chadema (Bavicha) limesema limeshtushwa na mjumbe wa kamati kuu ya chama hicho, Edward Lowassa kumpongeza Rais John Magufuli.

Akizungumza leo Alhamisi Januari 11, Katibu wa Bavicha, Julius Mwita amehoji Lowassa anapata wapi ujasiri wa kumpongeza Rais wakati nchi inakabiliwa na matukio mengi ya uvunjaji wa haki za binadamu.

"Unampongezaje Magufuli wakati serikali yake bado haijatoa tamko lolote tangu Mwanasheria wa Chadema, Tundu Lissu alivyopigwa risasi," amesema.

"Unampongeza vipi Magufuli wakati serikali yake imezuia mikutano ya vyama vya siasa."

 

Mwita amesema kitendo cha Lowassa kumpongeza Rais Magufuli kimewasikitisha hasa kutokana na mazingira ya kisiasa yalivyo hapa nchini.

"Vyama vya upinzani vina malalamiko mengi hatukutegemea kiongozi kusimama na kumpongeza mtu anayevikwamisha vyama vya siasa," amesema.