Bilioni 6 zatolewa na Uingereza kujenga shule Kagera

Waziri wa Elimu na mafunzo ya ufundi, Profesa Joyce Ndalichako

Muktasari:

Akizungumza na waandishi wa habari mapema leo Waziri wa Elimu na mafunzo ya ufundi Profesa Joyce Ndalichako amesema msaada huo utasaidia kujenga shule za Ihungo na Nyakato ambazo zimeharibika kwa kiasi kikubwa.

Dar es Salaam. Wizara ya Elimu  na mafunzo ya Ufundi Stadi,  imepokea  kiasi cha Shilingi  6.3bilioni kutoka kwa Shirika la Misaada na maendeleo la Uingereza (DFID) kwa ajili ya kufanyia ukarabati wa shule zilizoharibiwa na tetemeko la ardhi mkoani Kagera.

Akizungumza na waandishi wa habari mapema leo Waziri wa Elimu na mafunzo ya ufundi Profesa Joyce Ndalichako amesema msaada huo utasaidia kujenga shule za Ihungo na Nyakato ambazo zimeharibika kwa kiasi kikubwa.

"Shule hizo zitajengwa vizuri na kwa uimara zaidi ili kuzuia matatizo ya aina hiyo pindi yatapo tokea tena" amesema.

Amesema fedha hizo zimetolewa na shirika hilo mara moja hivyo ujenzi na ukarabati utaanza mara moja ili kuondoa adha wanayoipata wanafunzi.

"Utaratibu umeshafanyika na wakandarasi wanaendelea na taratibu ili kuanza ujenzi huo" amesema