Binti Karume ‘amchana’ Lipumba

Mtoto wa Rais wa zamani wa Zanzibar,Fatma Karume

Muktasari:

Fatma, mtoto wa Amani Abeid Karume ambaye ni rais wa sita wa Zanzibar, alisema hayo alipoulizwa kuhusu hali iliyoukumba uongozi kwenye chama hicho kikuu cha upinzani visiwani Zanzibar baada ya tamko la Msajili wa Vyama vya Siasa kuwa, anamtambua Profesa Lipumba kuwa mwenyekiti halali wa CUF.

Dar es Salaam. Fatma Karume, mtoto wa rais wa zamani wa Zanzibar, ameshangazwa na kitendo cha Profesa Ibrahim Lipumba  kutaka kurudi kwenye nafasi yake ya awali ya uenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) wakati alijiuzulu mwenyewe.

Fatma, mtoto wa Amani Abeid Karume ambaye ni rais wa sita wa Zanzibar, alisema hayo alipoulizwa kuhusu hali iliyoukumba uongozi kwenye chama hicho kikuu cha upinzani visiwani Zanzibar baada ya tamko la Msajili wa Vyama vya Siasa kuwa, anamtambua Profesa Lipumba kuwa mwenyekiti halali wa CUF.

Msajili huyo, Jaji Francis Mutungi alitoa uamuzi huo baada ya kuziita pande zinazosigana kwenye mgogoro, kusikiliza hoja zao baadaye kutoa maoni na msimamo wa ofisi yake kuwa Profesa Lipumba alifuta uamuzi wake kwa maandishi kabla ya mkutano mkuu wa CUF haujajadili barua yake ya kujiuzulu, hivyo anaendelea kuwa mwenyekiti halali.

“Profesa Lipumba alijiuzulu mwenyewe. Aliandika barua akaipeleka kwa katibu mkuu, kisha akautangazia umma na dunia nzima ikafahamu kwamba siyo tena mwenyekiti wa CUF,” alisema.