Boa Benki watoa mashine ya ujenzi wa ukuta Bahari ya Hindi

Muktasari:

Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa BOA, Wasia Mushi amesema makabidhiano ya mashine hiyo ni mpango wa benki hiyo kununua na kukodisha mitambo itakayowezesha wateja kufanya kazi bila kuwa na fedha taslimu.

Dar es Salaam. Benki ya Afrika (BOA), imetoa mashine ya ujenzi yenye thamani ya Sh300milioni kwa Kampuni ya Dezo Civil Contractors Ltd ili iweze kuharakisha ujenzi wa kuta kwenye Pwani ya Bahari ya Hindi katika Barabara ya Barack Obama jijini Dar es Salaam.

 

Akizungumza leo, Jumatatu, Julai 17, Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa BOA, Wasia Mushi amesema makabidhiano ya mashine hiyo ni mpango wa benki hiyo kununua na kukodisha mitambo ambayo inawezesha wateja kufanya kazi bila kuwa na fedha taslimu.

 

Amesema mpango huo utakuwa na tija kwa wajasiriamali wakubwa na wadogo ambao hawana mitaji ya kuendesha miradi mbalimbali.

 

Kwa upande wake, mhandisi wa kampuni hiyo, Kavuna Msina amesema mradi wa kujenga ukuta kwenye ufukwe huo utasaidia kuzuia mmomonyoko wa udongo kwenye barabara hiyo.

 

Amesema ujenzi huo ulioanza Desemba 2016 utakamilika Oktoba mwaka huu.

 

Amesema changamoto ni ukosefu wa vitendea kazi na akaishukuru benki hiyo kwa kuwakabidhi mashine hiyo.