Mwijage ateua wajumbe wanne bodi ya TFC

Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage 

Muktasari:

Bodi hiyo ambayo uteuzi wake umeanza Desemba Mosi, 2017 itafanya kazi kwa miaka mitatu.

Dar es Salaam. Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage amewateua wajumbe wa bodi ya wakurugenzi wa Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC).

Taarifa kwa umma ya leo Alhamisi Desemba 7,2017 iliyotolewa na Naibu Katibu Mkuu (Biashara na Uwekezaji), Profesa Joseph Buchweishaija imesema

uteuzi huo kwa kipindi cha miaka mitatu umeanza Desemba Mosi, 2017.

Uteuzi huo umefanyika baada ya jana Desemba 6,2017 Rais John Magufuli, kumteua Profesa Egid Mubofu kuwa mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi wa TFC kuanzia Desemba Mosi, 2017.

Wajumbe wa bodi walioteuliwa ni Nuru Angetile Ndile (Mchumi Mkuu, Wizara ya Fedha na Mipango);  Eli Nanyaro Pallangyo (Mkurugenzi Msaidizi, Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji); Dk Kadida R.S. Mashaushi (Mhadhiri, Chuo cha Usimamizi wa Fedha -IFM); na Peter Barnabas Shao (mshauri wa masuala ya fedha katika kilimo).

Taarifa imesema bodi hiyo itazinduliwa Desemba 11,2017 saa nne asubuhi katika ofisi za Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji mjini Dodoma.