Bomoabomoa kuikumba Serengeti Moshi

Lango la kuingia katika kiwanda cha Kampuni ya  Bia  ya Serengeti  eneo la Bomambuzi, Manispaa ya Moshi mkoani Kilimanjaro likiwa limewekwa alama ya X.

Muktasari:

  • Rahco imeweka alama ya X kwenye majengo katika maeneo mbalimbali nchini, ikielezwa yamejengwa kwenye eneo la reli.

Moshi. Kiwanda cha Bia cha Serengeti (SBL) ni miongoni mwa majengo yaliyowekwa alama ya X kuashiria kuwa yanapaswa kubomolewa kwa kuwa yapo eneo la reli.  

Timu ya Kampuni Hodhi ya Rasilimali za Reli (Rahco) imeweka alama maeneo mbalimbali likiwemo eneo hilo, wahusika wakipewa siku 30 kuondoka.

Kiwanda cha Serengeti kipo Kata ya Bomambuzi mjini Moshi.

Ofisa Uhusiano wa SBL, John Wanyancha amesema hana taarifa kamili kuhusu suala hilo.

Hata hivyo, amesema amejipanga pamoja na uongozi wa kiwanda kulifanyia uchunguzi.

Amesema alipokea taarifa kutoka kwa watumishi wa kiwanda leo Alhamisi saa tano asubuhi kuhusu uwekaji wa alama hizo unaoendelea. Ameahidi kutoa tamko kesho.

Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa ya Moshi, Michael Mwandezi amesema halmashauri haimiliki reli kwa kuwa ipo chini ya shirika la reli.

Mwandezi amesema yapo maeneo mawili yanayosadikiwa kuwa na hati miliki na  ameshaandaa timu kwa ajili ya kwenda kufanya uchunguzi kubaini kama yapo eneo la reli.

“Wataalamu wapo kwenye uchunguzi kubaini hati hizo ni za ukweli au la,” amesema.