Bulaya ashinda, awabwaga tena wapiga kura

Mbunge wa Bunda Mjini, Ester Bulaya.

Muktasari:

Mahakama imeziona hoja za warufani kuwa hazina msingi kwa sababu kasoro walizozilalamikia hazikuwa na athari katika matokeo ya uchaguzi.

Dar es Salaam. Mahakama ya Rufani imetupilia mbali rufaa dhidi ya Mbunge wa Bunda Mjini, Ester Bulaya.

Hukumu ya rufaa hiyo imesomwa leo Julai 28 na Naibu Msajili wa Mahakama hiyo, Elizabeth Mkwizu.

Wapiga kura hao, Magambo Masato, Matwiga Matwiga, Janes Ezekiel na Escietik Malagila walikata rufaa mahakamani hapo wakipinga hukumu ya Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza, iliyompa ushindi Bulaya katika kesi ya uchaguzi waliyoifungua wakipinga matokeo yaliyompa ushindi Bulaya katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.

Rufaa hiyo ilisikilizwa Mei 11 mwaka huu na jopo la majaji watatu wa Mahakama ya Rufani. 

Akisoma hukumu hiyo Naibu Msajili Mkwizu amesema kuwa hoja za warufani hao hazina msingi kwani kasoro walizokuwa wakizilalamikia hazikuwa na athari katika matokeo ya uchaguzi huo.