Bulyanhulu yafunguka, yaeleza sababu ya kumzuia RC

Muktasari:

Jana mkuu huyo wa mkoa alienda kwa ajili ya ukaguzi wa uzalishaji kwenye mgodi huo.

Kahama. Meneja Ufanisi na Maendeleo ya Jamii wa mgodi wa Bulyanhulu, Elias Kastila amesema kilichosababisha Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Terrack na msafara wake kushindwa kuingia ndani ya mgodi huo ni mfumo wa ulinzi unaotegeshwa muda maalumu usioweza kubadilika hadi muda huo ufike.

 

 Kastila amesema isingewezekana msafara huo kuingia mgodini kwa sababu mtambo huo maalumu wa ulinzi ulikuwa umetegeshwa kufunguka saa 12.00 asubuhi ya leo, Ijumaa.

 

Kwa misingi hiyo, Kastila  amesema hakukuwa na namna nyingine ya kufungua mlango wa kuingilia mgodini, labda kulipua kwa bomu au baruti.

 

Akizungumzia uamuzi wa Mkuu wa Mkoa kuweka ulinzi wa polisi kuzuia mtu kuingia wala kutoka mgodini, Kastila amesema huo umetokana lengo la kujiridhisha hakuna tu labda kuna njama za kutorosha mali, jambo alilosema uongozi wa mgodi hauwezi kufanya kwa sababu hakuna kitu cha kutorosha wala kuficha kutokana na shughuli zote kufanyika kwa uwazi na utaratibu unaoruhusiwa kisheria.

 

Kwa misingi hiyo, iwapo uongozi wa Serikali mkoani Shinyanga utataka kutembelea na kukagua shughuli mgodini hapo kama ilivyofanya kwa mgodi wa Buzwagi, basi ulipaswa kwenda eneo hilo kuanzia saa 12.00 asubuhi ya leo.