Bunge lamjibu Mbowe

Mwenyekiti wa Chadema,Freeman Mbowe

Muktasari:

  • Ofisi ya Bunge imesema imeshatoa fedha zilizochangwa na wabunge kusaidia gharama za matibabu ya Lissu.

Dar es Salaam. Ofisi ya Bunge imesema fedha zilizochangwa na wabunge Sh.43 milioni kwa ajili ya kusaidia matibabu ya Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu zimetumwa katika akaunti ya Hospitali ya Nairobi anakopatiwa matibabu.

Bunge limetoa taarifa kwa umma leo Ijumaa saa chache baada ya Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe kuzungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam na kueleza fedha hizo hazijatumwa.

Katika taarifa hiyo, Bunge limesema fedha hizo zimetumwa Septemba 20 kupitia Benki ya Barclays, Tawi la Hurlringham katika akaunti namba 045 1155318 yenye jina Kenya Hospital Association.

“Fedha hizi zingeweza kutumwa mapema zaidi isipokuwa mawasiliano yalikuwa yanafanyika kupata namba ya akaunti ya kutuma fedha hizo na taratibu nyingine za malipo nje ya nchi,” imesema taarifa ya Bunge.

Ofisi ya Bunge imewaomba Watanzania kila mmoja na imani yake kuendelea kumuombea Lissu ili apone haraka na kurejea nchini kuendelea na majukumu yake.

Baada ya Lissu kushambuliwa na kujeruhiwa kwa risasi Septemba 7 nyumbani kwake Area D mjini Dodoma akitokea bungeni, wabunge waliazimia kutoa nusu ya posho zao kugharimia matibabu.

Mwisho.