CAF yazibananisha Simba, Mtibwa

Muktasari:

Badiliko jingine ni lile la kutoa nafasi ya bingwa wa Ligi ya Mabingwa msimu wa 2018/2019 

Dar es Salaam. Mabadiliko ya kalenda za mashindano ya soka Afrika kwa ngazi ya klabu yamezitega timu mbili zitakazoiwakilisha Tanzania Bara kwenye mashindano ya kimataifa msimu ujao.

Tofauti na awamu zilizopita ambapo kalenda ya mashindano hayo ilikuwa inaanza Februari na kumalizika Novemba, awamu ijayo ya mashindano hayo itaanza Novemba mwaka huu na kumalizika Mei kama ilivyo mfumo wa uendeshaji wa mashindano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya na ligi mbalimbali za soka kwenye bara hilo.

Kwa mujibu wa barua ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) kwenda kwa nchi wanachama wake, mabadiliko hayo ya kalenda ya Ligi ya Mabingwa Afrika na Kombe la Shirikisho Afrika ni utekelezaji wa uamuzi uliofikiwa na Kamati ya Utendaji ya CAF, Januari 10 mwaka huu.

Mbali na hilo, badiliko jingine ni lile la kutoa nafasi ya bingwa wa Ligi ya Mabingwa msimu wa 2018/2019 kufuzu moja kwa moja kwenye mashindano yatakayofuata hata kama atafanya vibaya kwenye ligi ya nchini kwake.

Maelekezo mengine ambayo barua hiyo imeyatoa kwa nchi wanachama ni kuwa mechi zote za Ligi ya Mabingwa Afrika zitachezwa Ijumaa au Jumamosi, wakati mechi zote za Kombe la Shirikisho zinapaswa kuchezwa siku ya Jumapili tu.

Mabadiliko hayo moja kwa moja yatawagusa wawakilishi wa Tanzania kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika, Simba pamoja na Mtibwa ambayo inapaswa kushiriki Kombe la Shirikisho Afrika kwa sababu ligi zao za ndani kwa maana ya Ligi Kuu Tanzania Bara na Kombe la FA huchezwa kati ya Agosti na Mei na mara nyingi mechi zake kufanyika siki