CCM yaionyesha jeuri Ukawa

Muktasari:

Vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) na vingine vilivyo nje ya umoja huo vimejikuta katika wakati mgumu katika uchaguzi huo mdogo.

Dar/mikoani.  Chama cha Mapinduzi (CCM) kimeibuka kidedea katika uchaguzi wa ubunge Jimbo la Dimani, Zanzibar na kushinda viti vya udiwani katika maeneo mengi Tanzania Bara katika majimbo yaliyotoa matokeo yake mpaka jana usiku.


Vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) na vingine vilivyo nje ya umoja huo vimejikuta katika wakati mgumu katika uchaguzi huo mdogo.


CCM iliibuka mshindi katika uchaguzi wa Dimani uliotokana na jimbo kuwa wazi baada ya kifo cha mbunge wake Hafidh Ally Tahri kilichotokea Novemba mwaka jana mjini Dodoma, alikokuwa akihudhuria vikao vya Bunge.


Msimamizi wa uchaguzi katika Jimbo la Dimani, Fatma Gharib Haji alimtangaza mgombea wa CCM, Juma Ali Juma kuwa mshindi wa ubunge wa jimbo hilo kwa kupata kura 4,860 dhidi ya mpinzani wake Abdulrazak Khatib Ramadhani wa CUF aliyepata kura 1,234.