Chadema, Serikali wavutana kuhusu sheria

Msajili wa vyama vya siasa, Jaji Francis Mutungi

Muktasari:

Sheria hiyo imesababisha Chadema kufungua kesi Mahakama Kuu ikitaka itoe tafsiri baada ya Jeshi la Polisi kuzuia mkutano uliopangwa kufanyika Kahama na baadaye kutangaza kuzuia mikutano ya hadhara na maandamano kwa maelezo kuwa yanalenga kushawishi wananchi kutotii viongozi.

Dar es Salaam. Wakati wapinzani wakitumia Katiba, Sheria ya Vyama vya Siasa na Kanuni za Maadili kwa Vyama vya Siasa kutetea hoja yao kuwa wana haki ya kuendesha mikutano, Serikali imekuwa ikitumia amri ya Rais John Magufuli na sheria hizo kuzuia shughuli hizo.

Sheria hiyo imesababisha Chadema kufungua kesi Mahakama Kuu ikitaka itoe tafsiri baada ya Jeshi la Polisi kuzuia mkutano uliopangwa kufanyika Kahama na baadaye kutangaza kuzuia mikutano ya hadhara na maandamano kwa maelezo kuwa yanalenga kushawishi wananchi kutotii viongozi.

Mvutano huo umekolezwa baada ya Chadema kutangaza maandamano na mikutano kote nchini kupinga agizo la Rais Magufuli na polisi la kuzuia mikutano ya kisiasa, wakiita kuwa ni ukandamizaji wa demokrasia.

Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Profesa Mwesiga Baregu amesema waliangalia mara kadhaa tangazo walilolitoa kuhusu Ukuta na kubaini hakuna chembe ya uchochezi, kinyume na taarifa ya onyo aliyoitoa Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi.