Chadema yafafanua alikolazwa Lissu

Muktasari:

  • Chadema imesema awali walipanga Lissu akatibiwe katika Hospitali ya Aga Khan lakini hilo halikufanyika.

Dar es Salaam. Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimeeleza kuwa Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu aliyejeruhiwa kwa kupigwa risasi wiki iliyopita amelazwa katika Hospitali ya Nairobi nchini Kenya.

Chadema imetoa ufafanuzi huo baada ya taarifa za awali kueleza kuwa, Lissu anatibiwa katika Hospitali ya Aga Khan nchini humo.

Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Chadema, Tumaini Makene amesema leo Alhamisi kuwa, awali walipanga kumpeleka Hospitali ya Aga Khan lakini hilo lilibadilishwa baadaye.

Lissu alishambuliwa na kujeruhiwa kwa risasi Septemba 7 akiwa nyumbani kwake Area D mjini Dodoma na siku hiyohiyo alisafirishwa kupelekwa Nairobi.

Kabla ya kusafirishwa saa sita usiku, Lissu ambaye pia ni mwanasheria wa Chadema na Rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), alipatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Dodoma.