Clinton akataa kugombea tena urais

Muktasari:

Katika mahojiano yaliyorushwa moja kwa moja na kituo cha BBC Radio 4 nchini Uingereza, Clinton aliulizwa ikiwa atajitokeza tena kuwania urais na yeye alijibu: "Hapana, sitawania tena."

Washington, Marekani. Mwanamama Hillary Clinton amesisitiza tena kwamba hatagombea tena urais kwa mara ya tatu licha ya Rais Donald Trump kumtaka afanye hivyo kwa mara ya tatu.

Hillary ambaye ni mke wa aliyekuwa Rais wa Marekani Bill Clinton, aligombea urais kwa mara ya kwanza mwaka 2008 lakini aliangushwa na Barack Obama katika mchujo ndani ya chama cha Democratic. Mwaka 2016 alishinda uteuzi lakini aliangushwa na Trump katika uchaguzi uliofanyika Novemba 8.

Trump alishinda kinyang’anyiro cha kuishi ikulu kwa kura 306 za Majimbo ya Uchaguzi (Electoral College) dhidi ya 232 za Clinton ingawa mwanamama huyo ndiye aliyeshinda kura za makabwela kwa zaidi ya kura 2.9 milioni.

Katika mahojiano yaliyorushwa moja kwa moja na kituo cha BBC Radio 4 nchini Uingereza, Clinton aliulizwa ikiwa atajitokeza tena kuwania urais na yeye alijibu: "Hapana, sitawania tena."

Alisisitiza kwamba wajibu wake sasa utakuwa kuendelea kufuatilia na kumkosoa Trump akisema anaamini sauti yake itakuwa “na nguvu kwa kuwa hatawania tena."

Hii si mara ya kwanza mwanamama huyo kusema hatagombea tena urais lakini kauli hii ya sasa imekuja siku chache baada ya Trump kusema atapenda kupambana naye tena.

"Ooh, natumaini Hillary atagombea,” alisema wakati wa mkutano na waandishi wa habari katika viwanja vya Rose Garden vilivyoko ikulu Jumatatu mchana. “Je, atagombea tena? Natumaini hivyo. Hillary, tafadhari gombea tena.”

Mapema siku hiyo alituma ujumbe wenye hisia kama hizo kwa njia ya Twitter. “Hivi karibuni niliulizwa ikiwa Mhalifu Hillary Clinton atagombea urais mwaka 2020? Jibu langu lilikuwa, 'Nategemea hivyo!'" aliandika Trump asubuhi.