Dar yatoa msamaha wa ushuru wa mabango

Muktasari:

Uongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam umetoa msamaha wa ushuru kwa mabango ya matangazo ya vivutio vya utalii.

Uongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam umetoa msamaha wa ushuru wa mabango ya matangazo ya vivutio vya utalii ikiwa ni sehemu ya mchango wa mkoa katika kukuza utalii.

Ofisa Misitu Mkoa wa Dar es Salaam, Mariam Kitula amesema hayo leo Jumatano katika warsha ya wadau wa utalii wa kanda ya pwani.

Warsha hiyo inalenga kukusanya maoni kuhusu marekebisho ya Sera ya Taifa ya Utalii ya mwaka 1999.

Kitula amesema uamuzi huo ulifikiwa baada ya ofisi ya mkuu wa mkoa kufanya majadiliano na Bodi ya Utalii na kukubaliana kuruhusu mabango hayo bila kutozwa ushuru.

"Mkuu wa mkoa alitaka mabango ya utalii yawepo katika jiji lote, bodi wakasema hawawezi kutokana na gharama, tulirudi tukajadili tukaona ipo haja ya kufuta ushuru huo ili mtalii anapowasili uwanja wa ndege akute mabango yanayoonyesha vivutio vyetu," amesema.