Diamond azungumzia video ya wimbo wake wa Baila

Muktasari:

Baadhi ya watu wanadai video hiyo inafanana na video ya msanii Shah Rukh wa nchini India


Dar es Salaam. Msanii Naseeb Abdul maarufu Diamond Platnumz amefunguka baada ya baadhi ya watu kumponda kuwa video ya wimbo wake wa Baila aliyoiachia jana inafanana na ya wimbo wa Saans wa mwanamuziki Shah Rukh wa nchini India.

Jana Ijumaa Julai 13, 2018 kupitia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Instagram, Diamond ameandika kuhusu Shah Rukh, maelezo yaliyoashiria kuwa mkali huyo wa Bongo Fleva ni shabiki wa msanii huyo wa India.

Kupitia ukurasa huo Diamond amesema, “Licha ya vingi vinipavyo furaha lakini kuwa kwenye mapenzi ama kumpenda mtu ndio starehe yangu kubwa, na kama ujuavyo, unapokuwa na kajina wengi wanakuwa wanakupenda.”

" Wengine kwa dhati wengine kwa matamanio, ila inapotokea anipendae nami nikampenda, basi huyo hufaidi haswa mapenzi yangu na ndio maana mara nyingi inakuwaga ni ngumu sana wengi kunisahau pindi tutenganapo.”

Amesema ikitokea siku akakutana na mwanamke kabla ya kuianza safari ya mapenzi, hawezi kumueleza neno lolote zaidi ya kumuwekea wimbo huo wa Baila kwa maelezo kuwa maneno yote ya mapenzi yapo kwenye wimbo huo.

Wakati Diamond akiandika hayo, dada yake Esma Platnumz aliandika chini ya ujumbe huo  na kubainisha kuwa hakujua kama kaka yake hana mpenzi mpaka sasa.