JPM awatajia wafanyabiashara mambo mawili muhimu

Muktasari:

Ametoa kauli hiyo katika mkutano wa Baraza la Taifa la Biashara


Dar es Salaam. Rais John Magufuli amewatajia  wafanyabishara nchini mambo mawili muhimu akiwataka kutumia fursa za masoko ya ndani ili kukuza ajira na kupunguza uagizaji wa bidhaa kutoka nje.

Akizungumza leo Jumatatu Machi 19, 2018 katika mkutano wa 11 wa Baraza la Taifa la Biashara Ikulu Dar es Salaam, Dk Magufuli amesema mfanyabiashara yeyote atakayekutana na vikwazo katika uwekezaji huo atoe taarifa mapema na atachukua hatua kwa mteule wake aliyehusika.

Ametoa mfano wa fursa ya kuzalisha sare za wanafunzi na majeshi nchini.  

“Tukisema kwa mfano sare zote za wanafunzi kuanzia darasa la kwanza hadi la saba, kuanzia kidato cha kwanza hadi cha sita zizalishwe na viwanda vyetu vya ndani au tukaanza kuzalisha viatu vya Jeshi, tutashindwa nini,”amesema Rais Magufuli.

 

Amesema Kiwanda cha Mwatex kitakapoanza kuzalisha sare hizo za wanafunzi, itasaidia kulinda soko la ndani, kuongeza uzalishaji wa zao la pamba na kukuza ajira kwa wakulima.

“Niwaambe Watanzania wenzangu tuwe wazalendo, tukifanya hivyo tutakuwa tumejibu hoja nyingi kwa wakati mmoja, atakayewakwamisha mniambie, mie si ndio mwenyekiti wenu? Ili kusudi nimwambie na yeye akajaribu kufanya biashara,”amesema.