Facebook yasimamisha akaunti ya kampuni iliyompigia debe Uhuru

Muktasari:

Ripoti iliyotolewa mwaka jana na kampuni ya kimataifa ya masuala ya faragha yenye makao yake London, Uingereza, inayopigana haki ya faragha duniani, ilisema kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2017, kampuni ya Cambridge Analytica iliongoza kampeni za mtandao ambazo zililenga ama kumshambulia kiongozi wa Nasa Raila Odinga au kumpigia debe Rais Kenyatta.

 


Nairobi, Kenya. Mtandao maarufu wa Facebook umetangaza kusimamishwa kwa akaunti ya Strategic Communication Laboratories kampuni mama ya Cambridge Analytica, kampuni ya uchambuzi wa data inayotuhumiwa kuratibu kampeni za mgawanyiko kuelekea uchaguzi mkuu wa rais mwaka 2017 nchini

Kusimamishwa kwa akaunti hiyo kumetokana na kampuni ya Cambridge Analytica kukiuka sera zake, mtandao huo mkubwa wa mawasiliano ya kijamii ulisema katika taarifa yake Ijumaa.

Facebook imedai kwamba mnamo mwaka 2015 Cambridge Analytica ilipewa maelezo jinsi ya kutumia Facebook bila idhini kutoka mtandao huo kupitia kazi iliyofanywa kwa ushirikiano na Profesa wa Saikolojia ya Chuo Kikuu cha Cambridge aitwaye Dr Aleksandr Kogan.

"Profesa huyo alisema uongo na kukiuka sera zetu za jukwaa kwa kupitisha data kutoka kwenye programu ambayo ilikuwa ikitumia kuingia FB kwenda SCL / Cambridge Analytica, ambayo inafanya kazi za kisiasa, serikali na za kijeshi kote ulimwenguni. Pia alimpatia data Christopher Wyloe wa kampuni ya Teknolojia ya Eunoia," ilisema Facebook.

Ripoti iliyotolewa mwaka jana na kampuni ya kimataifa ya masuala ya faragha yenye makao yake London, Uingereza, inayopigana haki ya faragha duniani, ilisema kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2017, kampuni ya Cambridge Analytica iliongoza kampeni za mtandao ambazo zililenga ama kumshambulia kiongozi wa Nasa Raila Odinga au kumpigia debe Rais Kenyatta.

Facebook ilisema kuwa kampuni hiyo kipekee ilimfanyia kazi Rais Kenyatta wakati wa kampeni yake ya uchaguzi.

Cambridge Analytica ilikanusha madai na ikasema kuwa haikuhusika katika maudhui yoyote hasi ya kisiasa.