Familia ya Diamond yamwandikia ujumbe mzito Zari

Muktasari:

  • Wameandika kumsifia Zari akisherehekea siku yake ya kuzaliwa leo

Siku chache baada ya mwanamuziki Diamond Platnum kukiri kuwa amezaa na mwanamitindo Hamisa Mobetto familia yake imemwandikia ujumbe mzito mzazi mwenzake Zarina Hassan katika siku yake ya kuzaliwa anayoiadhimisha leo.

Diamond ndiye alikuwa wa kwanza kuandika ujumbe huo kupitia ukurasa wake wa Instagram akionyesha kumsifia mwanamke huyo na kumtakia heri katika siku yake ya kuzaliwa.

Ujumbe huo ulisomeka “Uzuri na urembo pengine ningetembea nikakuta baadhi wanao pia… lakini akili, hekima pamoja na roho yako kwenye shida na raha kwangu ndiyo kitu pekee kwangu kinachonifanya nikupende na kukuthamini zaidi kadiri siku zinavyozidi kwenda. Wanaposema kwenye kila mafanikio ya mwanaume kuna mwanamke imara nyuma hawamaanishi eti anayepika na kuosha vyombo ama kufua nguo kila siku. Ni mwanamke mwenye kuwa bega kwa bega na mpenzi kwenye shida na raha… Happy birthday General.”

Dada yake Diamond, Esma naye hakuwa nyuma alishusha ujumbe wake uliosomeka “Hawajui thamani yako kwa Naseeb walimtenda wengi mpaka kufikia kudharauliwa majina kibao wakampa Mungu akakushusha, akakuvuta mbali ulipo ili umfute machozi ambayo siku zote alikuwa anatamani aje mtu amfute. Ulimpa furaha na akili ya kuogopa nisitumie sana nikiweke akiba ili wanangu wawe katika maisha mazuri na familia yangu…ulimpa nguvu ya kupambana usiku na mchana yote kwa ajili yenu. Mwanamke anayejua thamani ya mwanaume uko mbali lakini pindi urudipo unahakikisha anakula, anavaa na analala sehemu safi tena kwa mikono yako. Najua wengi wanataka nafasi yako ila hawawezi kuipata utaendelea kuwa Mama Tee hakuna kama wewe General”

Siku mbili zilizopita mama yake Diamond amekuwa akiweka picha za Zari akiwa amevaa zawadi alizomnunulia ambazo ni gauni na mtandio.

Zari pia aliweka picha hizo kwenye ukurasa wake na kuandika maneno yaliyosomeka, “Usidanganyike na gauni la malkia nililovaa, kwa ndani ni Meja Jenerali.”