Freeman Mbowe adondoka ghafla, alazwa Muhimbili

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe

Muktasari:

Jeremiah Mtobesya ambaye ni wakili wa Mbowe, aliiambia Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu

Dar es Salaam. Mahakama imeambiwa kuwa mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amelazwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili baada ya kudondoka ghafla alfajiri.

Jeremiah Mtobesya ambaye ni wakili wa Mbowe, aliiambia Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbard Mashauri, kuwa mteja wake alianguka leo Juni 18 akiwa nyumbani kwake.

Kadhalika, Mahakama imeelezwa kuwa Mbowe ambaye pia ni mbunge wa Hai, amefiwa na kaka yake, Henry Mbowe.

Akiwasilisha taarifa hiyo, Wakili Mtobesya alieleza kuwa Mbowe ambaye ni mshtakiwa namba moja katika kesi namba 112 ya 2018 amefiwa na kaka yake usiku wa kuamkia leo.

Awali Wakili wa Serikali Mkuu, Faraja Nchimbi aliiambia mahakama kuwa kesi ilipangwa kwa ajili ya washtakiwa Mbowe na wenzake wanane kusomewa maelezo ya awali PH na kwamba wamejiandaa na wapo tayari.

Hata hivyo aliiambia mahakama kuwa Juni 12 na 14 , 2018 walipokea mapingamizi ya kisheria na kwamba wapo tayari kuendelea na mapingamizi hayo.