Gambo amshukuru JPM kuongeza nguvu ujenzi wa kituo cha afya

Muktasari:

  • Gambo alisema hayo jana eneo la Kwamrombo, Kata ya Murriet kwenye kampeni za kumnadi mgombea udiwani wa Kata ya Murriet, Francis Mbise (CCM).

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo amemshukuru Rais John Magufuli kwa kuahidi kutoa Sh700 milioni za kuendeleza ujenzi wa kituo kikubwa cha afya cha Kata ya Murriet pamoja na ujenzi wa nyumba saba za askari.

Gambo alisema hayo jana eneo la Kwamrombo, Kata ya Murriet kwenye kampeni za kumnadi mgombea udiwani wa Kata ya Murriet, Francis Mbise (CCM).

Alisema anashukuru Rais Magufuli kwa kutoa msaada wa fedha hizo baada ya kuona juhudi kubwa zilizofanywa naye pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Arusha, Gabriel Daqqaro na Mkurugenzi wa Jiji la Arusha, Athumani Kihamia ili kuleta maendeleo.

Alisema fedha hizo alizozitoa zitajenga nyumba za polisi saba katika eneo hilo linalojengwa kituo cha polisi kitakachohudumia wananchi wa kata hiyo.