Gwajima: Mimi ni sababu ya Clouds kuvamiwa

Askofu wa kanisa la Ufufuo na uzima Joseph Gwajima

Muktasari:

Hatua ya Gwajima imekuja baada ya tukio la kituo hicho kuvamiwa na mkuu wa mkoa wa Dar es salaam Paul Makonda akiwa na polisi wenye silaha.

Dar es Salaam. Askofu wa kanisa la Ufufuo na uzima Joseph Gwajima amezungumza na waandishi wa habari  wa Clouds Media Group  na kusema kilichomfanya afike katika ofisi hizo ni kutoa pole kwa kuwa yeye ni sehemu ya sababu za uvamizi huo.

“Isingekuwa busara watu wavamiwe na mimi ni mhusika mkuu halafu nisije kutoa pole,” alisema

Hatua ya Gwajima imekuja baada ya tukio la kituo hicho kuvamiwa na mkuu wa mkoa wa Dar es salaam Paul Makonda akiwa na polisi wenye silaha.

Gwajima amewasilia saa 4:00 asubuhi akiwa na msafara wa magari zaidi ya manne na walinzi wake takribani 30 na alipofika alipokelewa na Mkurugenzi wa vipindi na Uzalishaji Ruge Mutahaba na kufanya mazungumzo na waandishi wa habari  na baadaye na uongozi wa kituo hicho.

Amewataka Clouds kuendelea na kazi zao za kawaida na kutaka suala hilo lisichukuliwe kisiasa huku akikisitiza kuwa Mkuu wa mkoa alikosea.