Haji Manara, wadau wa michezo wazungumzia kupatikana Mo Dewji

Muktasari:

Wadau wa soka nchini Tanzania wamezungumzia kupatikana kwa mfanyabiashara na mwekezaji wa klabu ya Simba, Mohammed Dewji ‘Mo Dewji’ leo baada ya kutekwa na watu wasiojulikana siku nane zilizopita


Dar es Salaam. Wadau wa soka nchini wamezungumzia kupatikana kwa mfanyabiashara na mwekezaji wa klabu ya Simba, Mohammed Dewji ‘Mo Dewji’ leo baada ya kutekwa na watu wasiojulikana siku nane zilizopita.

Wakizunguza na MCL Digital kwa nyakati tofauti, Katibu Mkuu wa zamani wa Shirikisho la soka Tanzania (TFF),  Fredrick Mwakalebela amesema Mo Dewji kurejea akiwa mzima wa afya kutaleta chachu ya maendeleo katika soka.

“Mo katika soka si Simba tu bali ni muhimu kwa nchi nzima kutokana na kujitolea kwake kwa hiyo kurejea kwake akiwa mzima wa afya ni faraja kwa nchi hasa upande wa michezo,” amesema Mwakalebela.

Msemaji wa klabu ya Simba Haji Manara katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Twitter ameandika, “Naandika nafuta, naandika nafuta, ahh!! Anaitwa Mungu Mwenye enzi. Alhamdulillah!! Ngoja nitulize akili kwanza nitarudi baadaye.”

Naye  kocha msaidizi wa timu ya Taifa ya wanawake Twiga Stars, Edna Lema amesema kurudi kwa Mo Dewji kumerudisha furaha kwa mashabiki na viongozi wa soka nchini.

Amesema alivyokosekana wachezaji wa Simba hata viongozi wa klabu hiyo hawakuwa katika saikolojia nzuri.

"Kurudi kwake kutaongeza morali kwa wapenzi wote wa soka haswa wa Simba na hata wachezaji wa klabu hiyo watakuwa katika hali  nzuri ya kushindana," amesema Lema.

"Watu wote tulikuwa tunaomba arudi salama na imekuwa hivyo tunaomba asiache moyo wake wa kuendeleza michezo kutokana na changamoto hii ambayo amekutana nayo,” amesema.