Hakimu agoma kujitoa kesi ya Nondo

Muktasari:

Jana Mei 15, 2018 Nondo aliiandikia barua Mahakama kumkataa hakimu 

Iringa. Hakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Iringa, John Mpitanjia anayeendesha kesi inayomkabili mwanafunzi wa mwaka wa tatu Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM), Abdul Nondo amegoma kujitoa katika kesi hiyo kwa maelezo kuwa malalamiko ya mshtakiwa anayetaka ajitoe, hayana ushahidi wa kutosha.

Jana Mei 15, 2018 Nondo aliiandikia barua Mahakama hiyo kumkataa hakimu huyo anayesikiliza shauri lake, kwamba anamtilia shaka na ameona aiandike barua Mahakama ili itende haki.

Leo Mei 16, 2018 akitoa uamuzi huo mdogo wa Mahakama, Mpitanjia amesema mahakama ni chombo cha mwisho cha kutenda haki  hivyo itaangalia usawa kwa pande zote mbili ikiwa ni sambamba na kutoa haki kwa wakati bila kufungamana na upande wowote.

Baada ya kutoa muamuzi huo hakimu aliamuru upande wa jamuhuri kuendelea kutoa ushahidi wa mashahidi waliobaki katika kesi hiyo.