Halmashauri inahitaji tani 12, 526 za chakula

Shinyanga. Halmashauri   ya Wilaya ya Shinyanga inahitaji tani 12,526 za chakula kunusuru maisha ya watu 111,340 wanaokabiliwa na upungufu wa chakula katika wilaya hiyo.

 

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga Ngassa Mboja katika kikao cha baraza la Madiwani kilichofanyika jana chakula hicho kinatakiwa kutumika hadi  Juni 2017 hadi February 2018.

 

Mboje amesema tathimini ya hali ya chakula iliyofanywa na timu ya uchambuzi wa chakula na lishe ya Wilaya hiyo (MUCHALI) kwa kuzingatia miongozo na taratibu za tathimini ilibaini upungufu huo.

 Amesema tathimini na uchambuzi wa MUCHALI ulionyesha kuwa jumla ya kaya 18,557 zenye idadi ya watu 111,340 zinahitaji tani 12, 526 za chakula kwa kipindi cha miezi tisa ijayo.

 

Wakijadili taarifa hiyo madiwani wa halmashauri hiyo wamesema upungufu wa chakula unalikabili eneo  lote la halmashauri nzima na kuomba kamati ya MUCHALI irudie kufanya tathimini upya na kwa makini ili kuleta takwimu zitakazokidhi mahitaji ya chakula kwa wilaya yote.

 

Akizungumza kwa jazba diwani wa kata ya Solwa Awadhi Aboud alisema baadhi ya wananchi wanakunywa uji na baadhi yao  wanakula mlo mmoja kwa siku jambo ambalo halikubaliki.

 

“Ndugu zangu mimi sitanii hata kidogo katika kata yangu nina mama mmoja ana watoto saba hadi sasa ana miezi mitatu yuko nyumbani kwangu kupata huduma ya chakula na watoto wake, lakini leo ni mwezi wa tano, je mwezi wa 12 mwaka huu hali itakuwaje?”  Amehoji Aboud.