Hamisa Mobetto adai ‘matusi mtandaoni’ yamemnufaisha kimtindo

Hamisa Mobetto

Muktasari:

Amesema yeye ni miongoni mwa wenye mioyo migumu kiasi cha kutoumizwa na maneno ya watu.


Kama unafikiri mwanamitindo Hamisa Mobetto anatikiswa na mambo yanayozungumzwa mitandaoni utakuwa unakosea.

Mrembo huyu ameweka wazi kuwa hatikiswi na maneno hayo kwani alishazoea kuzungumziwa tangu utotoni.

“Mimi huwa naangalia mtandaoni nikikuta matusi namblock mtu aliyefanya hivyo kwa sababu matusi hayakubaliki katika jamii yetu, suala la kuzungumziwa wala sishangai tangu nikiwa mdogo watu walikuwa wakinizungumzia, mama akawa ananiambia ‘am so special’,”

Amesema yeye ni miongoni mwa wenye mioyo migumu kiasi cha kutoumizwa na maneno ya watu.

Amesema licha ya changamoto nyingi anazokutana nazo kwenye mitandao ya kijamii, imemsaidia kufanikiwa.

Hamisa ambaye pia ni mmiliki wa duka la mitindo la Mobettostyle amesema maendeleo hayo ya teknolojia yamekuwa na matokeo hasi na chanya kwake.

Akizungumza muda mfupi baada ya kuzinduliwa kwa kampeni ya kuhamasisha matumizi sahihi ya vijana ya ‘Be Smart’, Hamisa amesema amefanikisha vingi kupitia mitandao.

Amefafanua kuwa hata duka lake linafanya vizuri kwa sababu anatumia vyema ukurasa wake wa Instagram kulitangaza.

“Mimi ni mnufaika na muathirika wa mitandao, kwa upande wa athari nakutana na changamoto nyingi ikiwemo kutukanwa na watu ambao hata siwafahamu,

“Kwenye faida huko ni kuzuri zaidi maana hata duka langu limekuwa kwa sababu ya Instagram, si kwamba ni bora zaidi kuliko mengine ila nalitangaza sana,” anafafanua.

Mwanamitindo huyu ambaye amewahi kushiriki mashindano ya Miss Tanzania amekuwa gumzo mitandaoni tangu mwaka jana baada ya kuwapo tetesi kuwa ana uhusiano wa kimapenzi na mwanamuziki Diamond Platnumz.

Aliendelea kuwa gumzo baada ya mwanamuziki huyo kukiri kuwa baba wa mtoto wa mlimbwende huyo, Dylan mwenye umri wa mwaka mmoja na miezi miwili.

Hamisa ambaye pia ni balozi wa bidhaa za nywele za Prima, amekuwa gumzo baada ya kuwapo makundi (team) ‘zinazowapigania’ watu maarufu nchini kama vile Team Wema, Team Mobetto na Team Zari.

Mashabiki wa makundi yote haya wamekuwa wakichuana mtandaoni kuwapigania wanaowakubali na hapa ndipo watu maarufu hutengeneza ufuasi mkubwa.

Hamisa ni miongoni mwa mastaa wenye ufuasi mkubwa nchini akiwa na wafuasi milioni 2.5 katika mtandao wa Instagram.

Elizabeth Edward