VIDEO: Hanspope, Lauwo watakiwa kuripoti Takukuru

Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Brigedia Jenerali, John Mbungo

Muktasari:

  • Hanspope na Lauwo wametajwa katika sakata la ununuzi na uwekaji wa nyasi bandia kwa ajili ya uwanja wa klabu ya Simba uliopo Bunju jijini Dar es Salaam.

Dar es Salaam. Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) imemtaka Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya klabu ya Simba, Zacharia Hanspope kuripoti katika ofisi za taasisi hiyo au polisi kujibu tuhuma zinazomkabili.

Mbali na Hanspope, aliyekuwa mwenyekiti wa Simba,  Franklin Lauwo naye ametakiwa kujisalimisha.

Kauli hiyo imetolewa leo Ijumaa Septemba 14, 2018 na naibu mkurugenzi mkuu wa Takukuru, Brigedia Jenerali, John Mbungo katika mkutano wake na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.

Amedai kuwa Hanspope alitoa taarifa za uongo kuhusu malipo ya kodi.

Amesema Zacharia kwa kushirikiana na washtakiwa wengine Evans Aveva, Geofrey Nyange 'Kaburu' walitoa maelezo ya uongo kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwamba klabu ya Simba imenunua nyasi bandia kutoka Kampuni ya Ninah Guangzhou Trading zenye thamani ya Dola 40,577  za Marekani, maelezo ambayo yalikuwa ya uongo kwani nyasi hizo zilinunuliwa kwa dola 109,499.

Kuhusu Lauwo, Mbungo amesema alifanya kazi ya ukandarasi wa ujenzi wa uwanja wa mpira wa miguu wa Simba uliopo Bunju, Kinondoni jijini Dar es Salaam kwa Sh249, 929,704 wakati akiwa hajasajiliwa katika Bodi ya Makandarasi Tanzania.

"Tumewatafuta kwa njia za siri na uwazi bila mafanikio. Tunawataka kuripoti kituo cha Takukuru au polisi,"amesema Mbungo.

"Mwananchi atakayefanikisha kupatikana kwa watu hawa atapatiwa zawadi.”

Amesema kwa taarifa walizonazo, Hanspope aliondoka nchini kwenda Mombasa, Kenya, “kisha akaenda nchi zingine na kuna taarifa yupo hapa nchini amejificha. Tunamtaka yeye na mwenzake wajisalimishe. "

Amesema katika uchunguzi, Hanspope  ameonekana kuwa na hati tatu za kusafiria ambazo ni ya Afrika Mashariki na mbili za Tanzania zenye namba tofauti.