Hatima kesi ya mkurugenzi wa Jamii Forum Mei 28 mwaka huu

Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jamii Forum, Maxence Melo

Muktasari:

Siku hiyo Mahakama itaeleza kama mkurugenzi huyo na mwenzake wana kesi ya kujibu ama la

Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imepanga Mei 28, 2018 kutoa uamuzi  kama Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jamii Forum, Maxence Melo na mwenzake wana kesi ya kujibu au la.

 Uamuzi huo wa Mahakama umetolewa leo Mei 22, 2018 na Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama hiyo, Godfrey Mwambapa baada ya upande wa mashtaka kufunga ushahidi wao.

 Katika kesi hiyo ya jinai namba 457/2016, Melo na mwanahisa wa  mtandao huo, Micke William wanakabiliwa na shtaka la kushindwa kutoka ushurikiano kwa Jeshi la  Polisi  kwa kuzuia taarifa binafsi za wateja wao.

 

Awali, Wakili wa Serikali, Batilda Mushi amedai mahakamani hapo kuwa kesi hiyo imekuja kwa ajili ya uamuzi.

 Baada ya maelezo hayo, Hakimu  Mwambapa ameahirisha kesi hiyo hadi, Mei 28 atakapotoa uamuzi dhidi ya Mello na mwenzake kama wanakesi ya kujibu au laa.

 Tayari mashahidi wawili  wa upande wa Jamhuri wameshatoa ushahidi wao mahakamani hapo dhidi ya washtakiwa.

 Katika kesi ya msingi, Micke na Melo, wanadaiwa kuwa  kati ya Mei 10 na Desemba 13,2016 , kwenye eneo  la Mikocheni, wakiwa Wakurugenzi wa Mtandao wa Jamii  Media Co Ltd ambao unaendesha tovuti ya Jamii Forums wakijua Jeshi la Polisi Tanzania linafanya uchunguzi kuhusiana na mawasiliano ya kimtandao yaliyochapishwa katika tovuti yao kwa njia ya kuzuia uchunguzi huo, walishindwa kutekeleza amri ya kutoa data walizonazo.