IGP Sirro alipongeza Jeshi la Polisi Singida
Muktasari:
IGP Sirro ametoa pongezi hizo leo asubuhi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kweye viwanja vya kambi ya Kikosi cha Kuzuia Fujo (FFU) mjini hapa.
Singida. Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Simon Sirro amelipongeza Jeshi la Polisi mkoani Singida kwa juhudi zake za kupunguza matukio ya uhalifu yakiwamo ya utekeji wa magari.
IGP Sirro ametoa pongezi hizo leo asubuhi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kweye viwanja vya kambi ya Kikosi cha Kuzuia Fujo (FFU) mjini hapa.
Amesema matukio ya uhalifu mbalimbali mkoani Singida yamekuwa yakipungua kwa kiwango kikubwa kwa sasa, ikilinganishwa na miaka ya nyuma.
“Hatua hii inachangia uwepo wa amani na utulivu kwa wananchi wa mkoa wa Singida hivyo kutoa fursa za kujiletea maendeleo yao ya mkoa na taifa kwa ujumla,” amesema.
IGP Sirro amesema mafanikio hayo yamechangiwa na wananchi kwa kiwango kikubwa kwa ushirikiano wanaoutoa kwa Jeshi la Polisi.
Akifafanua amesema wananchi wamekuwa wakitoa taarifa sahihi na kwa wakati kwa Jeshi la Polisi pindi wanapobaini dalili ama matukio ya kihalifu.
“Kwa sasa kwa kweli wananchi hata ninyi waandishi mnatupa ushirikiano mzuri ambao unachangia kazi zetu kuwa nyepesi na za mafanikio makubwa. Sasa kule Kibiti mkoani Pwani, wananchi wanatusaidia mno taarifa zinazohusu mauaji ya watu wasiokuwa na hatia,” amefafanua zaidi.
IGP Sirro amesema kwa sasa Tanzania inaonewa wivu na nchi jirani kwa namna ilivyodhibiti matukio ya kihalifu na kupelekea nchi kuendelea kudumisha amani na utulivu.
Wakati huo huo, IGP Sirro ametumia fursa hiyo kuwaomba wananchi waendelee kushirikiana na jeshi hilo, kufichua baadhi ya watu wanaojihusisha na matukio mbalimbali ya kihalifu ili waweze kuchukuliwa hatua stahiki.