Idadi ya wanaofanya miamala kwa njia ya simu yaongezeka Tanzania na Kenya

Dar es Salam. Tanzania na Kenya zimetajwa kuwa nchi zenye ongezeko kubwa la matumizi ya huduma za kibenki kwa njia ya simu (simbanking) kwa mwaka 2016.

Mafanikio hayo yametokana na ongezeko la watumiaji wa huduma hizo kwa zaidi ya asilimia 40 katika nchi za ukanda huo kwa mujibu wa ripoti ya Shirikisho la Kampuni za Simu (GSMA).

Akizungumza leo Julai 14, juu ya maendeleo hayo, Mkurugenzi wa Biashara wa Vodacom hapa nchini, Sitoyo Lopokoiyit amesema kuwa hatua hiyo inatokana na kuwapo kwa sera zinazohimiza uvumbuzi na uwekezaji.

Amesema kuwa huduma za M-pesa zimeongezeka kwa asilimia 20 mwaka huu na kwamba huduma zimeendelea kuboreshwa ili kuendana na mahitaji ya wateja.

"Tumezidi kuboresha huduma za kimataifa na kupungiza gharama,hii ni safari kubwa na inahitaji ushirikiano kati ya wadau wa sekta hii,"amesema.

GSMA imeeleza kuwa hadi Desemba 2016, kulikuwa na jumla ya akaunti za simu 277 na jumla ya miamala 43 milioni hufanyika kila siku.