JKT kufufua viwanda nchini

Muktasari:

Akizungumza wakati wa mahafali ya kozi ya ukamanda na unadhimu mkoani hapa, Dk Mwinyi alisema viwanda watakavyohakikisha vinakuwepo ni pamoja na kiwanda cha Mzinga, Nyumbu na Suma JKT ambavyo vitafufuliwa ili vianze kuchangia pato la Taifa

Waziri wa Ulinzi na Jeshi  la Kujenga Taifa, Dk Hussein Mwinyi, amesema Jeshi la Kujenga Taifa (JKT)  limejipanga kutekeleza sera ya Serikali kwa kufufua viwanda nchini.

Akizungumza wakati wa mahafali ya kozi ya ukamanda na unadhimu mkoani hapa, Dk Mwinyi alisema viwanda watakavyohakikisha vinakuwepo ni pamoja na kiwanda cha Mzinga, Nyumbu na Suma JKT ambavyo vitafufuliwa ili vianze kuchangia pato la Taifa

Mara baada ya kutoa vyeti kwa wahitimu 41 wa kozi ya ukamanda na unadhimu kutoka nchi 10 za Ukanda wa Afrika Mshariki na SADC, Dk Mwinyi amesema, jeshi hilo limejipanga kuwawezesha askari kujiendeleza kielimu ili kumudu matumizi ya teknolojia za kisasa zinazokuwa siku hadi siku.

Amesema pia mpango ulioko sasa ni kuhakikisha Jeshi la Wananchi wa Tanzania linajipatia sifa kubwa kitaifa na  kimataifa katika utelekezaji wa majukumu yake ikiwa ni pamoja na kuhakikisha utendaji kazi wake wote unajitosheleza kwenye nyanja zote.

Mkuu  wa  chuo  hicho cha  Ukamanda na Unadhimu cha  Duluti, Meja Harrison Joseph Masebo, amesema chuo  hicho kinapokea na kufundisha maofisa wenye cheo cha meja hadi luteni ambao wanaandaliwa kuwa viongozi na makamanda wa ngazi mbalimbali.

"Licha ya kutoa mafunzo pia ni jukumu letu kuwajengea uwezo wa kutoa maamuzi chanya wakati wa amani na  wakati wa vita," amesema.

Maofisa waliohitimu wanatoka katika nchi kumi za SADC ikiwemo Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Msumbiji, Zambia, Namibia, Zimbabwe na Afrika Kusini.