JPM awaapisha makatibu wakuu, mabalozi wapya

Dar es Salaam. Rais John Magufuli amewaapisha viongozi mbalimbali walioteuliwa hivi karibuni akiwamo Rajab Luhwavi anayekuwa Balozi wa Tanzania, Msumbiji.

Taarifa iliyotumwa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Ikulu imesema wengine walioapishwa ni Tixon Nzunda aliyeteuliwa kuwa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) - anayeshughulikia Elimu.

Wengine ni Bernard Makali ambaye ameapishwa kuwa Katibu Tawala Mkoa wa Rukwa na Clifford Tandari, kuwa Katibu Tawala Mkoa wa Morogoro.

Pia Rais Magufuli amemuapisha Geoffrey Mwambe kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC).

“Viongozi wote walioapishwa wameahidi kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi wa hali ya juu katika kuwaletea wananchi maendeleo,” inasema taarifa hiyo

Hafla ya kuapishwa viongozi hao imehudhuriwa na Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan,Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki   Augustine Mahiga na viongozi mbalimbali wa Serikali.