Jengo la Tanesco Ubungo, lapigwa X

Dar es Salaam. Jengo la Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) limeshawekwa alama ya X ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Rais John Magufuli kulibomoa kupisha barabara za juu (Tazara Fly-Over).

Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) Mkoa wa Dar es Salaam, Ndyamukama Julius alisema jana kuwa pia, wametoa siku 30 kuhamisha ofisi hizo kabla ya kuanza kulibomoa.

Hivi karibuni, Rais Magufuli baada ya kukagua ujenzi wa barabara ya juu eneo la Tazara na Ubungo Interchange wakati akirejea Dar es Salaam kutoka kijijini kwake Chato mkoani Geita, aliagiza Tanroads kuvunja sehemu ya jengo la makao makuu ya Tanesco na la Wizara ya Maji na Umwagiliaji yaliyopo katika hifadhi ya barabara.

Wakati huohuo, Tanesco ilitoa taarifa jana ikiwahakikishia wateja kuwa utekelezaji wa agizo la Rais Magufuli hautaathiri huduma za umeme.