Kaburi lafukuliwa, maiti yaibwa

File Photo

Muktasari:

Maiti ya Elias Baswedi (33) iliyozikwa kwa taratibu zote kwenye mji huo, imefukuliwa na kuibwa kabla ya kupatikana baadaye porini ikiwa imekatwa mguu.

Chunya. Wakazi wa kitongoji cha Malangamilo kwenye mji mdogo wa Makongolosi wilayani hapa, wameingiwa kiwewe  baada ya kubaini kaburi la mtu waliyemzika limefukuliwa na mwili kuibwa.

Maiti ya Elias Baswedi (33) iliyozikwa kwa taratibu zote kwenye mji huo, imefukuliwa na kuibwa kabla ya kupatikana baadaye porini ikiwa imekatwa mguu.

Baswedi alifariki dunia baada ya kupigwa na kuchomwa moto na watu wasiojulikana Ijumaa usiku na alizikwa na ndugu zake baada ya kupata kibali cha polisi.

Siku mbili baada ya maziko, baadhi ya wakazi waliopita eneo alipozikwa walishangaa kuona kaburi likiwa limefukuliwa na ndani yake hakukuwamo maiti na vitu walivyomzika navyo kama vile sanda na mkeka.

Pangapanga Baswedi ambaye ni kaka wa marehemu, amesema tukio hilo liliwaongezea uchungu na walitoa taarifa polisi kwa ajili ya kuwasaka waliotoweka na maiti hiyo.

Mwili huo baadaye ulipatikana porini ukiwa umekatwa mguu.