Kamanda Muroto asisitiza madereva watukutu ‘watapata tabu sana’

Kamanda wa Polisi mkoa wa Dodoma Gilles Muroto 

Muktasari:

Amesema hayupo tayari kuona ukamanda wake ukichukuliwa kwani anaupenda na ni mtamu.


Dodoma. Kamanda wa Polisi mkoa wa Dodoma Gilles Muroto amesema kuanzia sasa madereva watakaovunja sheria kwa makusudi watapelekwa mahakamani badala ya faini ambazo nyingi huwaangukia matajiri wao.

Katika mkutano wake na madereva wa magari ya mikoani leo Julai 12, Muroto (maarufu ‘Watapata tabu sana’) amesema makosa mengi husababishwa na uzembe wa madereva lakini wanaoumizwa ni wamiliki kwa kulipa faini.

Amewataka madereva wote kutii sheria bila ya shuruti kwa kuwa polisi hawatakuwa na huruma katika kipindi hiki huku akisema hayuko tayari kuona ukamanda wake ukichukuliwa kwa sababu yoyote kwani anaupenda na ni mtamu.

Amesema ajali nyingi zimekuwa zikisababishwa na uzembe wa watumiaji wa barabara hasa madereva jambo alilosema amepanga vikosi vyake ili kuhakikisha Dodoma inaendelea kuwa salama.

“Lazima mcheze na mdundo wa ngoma, nataka mfanane na mti ambao hunesa wakati wa upepo na upepo ukitoka una imama, lakini mkikauka kama mpapai lazima mtavunjika tu,”amesema Muroto huku akichombeza maneno yake; ‘mtapata tabu sana’.