CC ya Chadema kesho Jumamosi

Muktasari:

Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kesho inakutana katika kikao cha ‘dharura’ jijini Dar es Salaam

Dar es Salaam. Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kesho inakutana katika kikao cha ‘dharura’ jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na Mwananchi leo Ijumaa Januari 12, 2018, Naibu Katibu Mkuu wa Chadema-Zanzibar, Salum Mwalimu amesema lengo la kikao hicho ni kufanya tathmini ya hali ya kisiasa nchini.

Mwananchi lilipotaka kujua kama lengo la kikao hicho ni kujadili ziara ya waziri mkuu wa zamani, Edward Lowassa kwenda Ikulu, Mwalimu amesema kikao hicho si cha dharura kwani kilipangwa kufanyika Desemba mwaka jana lakini kiliahirishwa kutokana na sikukuu za mwisho wa mwaka.

Amesema ajenda za kikao hicho zilipangwa kabla Lowassa ambaye ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema hajaenda Ikulu hivyo hakika uhusiano na ziara hiyo ila huenda jambo hilo likajitokeza.

“Suala hilo halipo kwenye ajenda ila linaweza kujitokeza na likijitokeza litazungumziwa lisipojitokeza basi,” amesema Mwalimu na kuongeza;

“Hata hivyo kwa upande wake inaweza kuwa fursa nzuri kuielezea Kamati Kuu na viongozi wenzake nini kilitokea.”