Idadi ya abiria yaanza kuongezeka Ubungo

Muktasari:

Sumatra imetangaza kutoa leseni za muda mfupi katika kipindi cha mwisho wa mwaka. 

Dar es Salaam. Askari wa usalama barabarani wamezuia magari zaidi ya 10 kufanya safari za mikoani kwa ajili ya ukaguzi katika kituo kikuu cha mabasi cha Ubungo jijini Dar es Salaam.

Mkuu wa Usalama Barabarani Ubungo, Said Ibrahimu akizungumza na MCL Digital leo Jumanne Desemba 12,2017 amesema wanaendelea na ukaguzi na kwamba magari yaliyozuiwa ni mabovu.

Katika kituo hicho idadi ya abiria imeongezeka ikielezwa ni kutokana na sherehe za mwishoni mwa mwaka.

Mamlaka ya Udhibiti Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra) jana Jumatatu Desemba 11,2017 kupitia taarifa kwa umma imetangaza kutoa leseni za muda mfupi katika kipindi cha mwisho wa mwaka.

Sumatra imewaalika wamiliki wenye mabasi ya ziada kuwasilisha maombi ya leseni za muda mfupi kwa ajili ya kuongeza huduma katika njia za mikoani zenye mahitaji zaidi kipindi hiki cha sikukuu za mwisho wa mwaka.

Mamlaka hiyo pia imewakumbusha wananchi wanaotarajia kusafiri kwa ajili ya mapumziko ya sikukuu za Krismasi na Mwaka Mpya kupanga safari mapema ili kuepusha usumbufu unaotokana na changamoto za usafiri.