Katibu Chadema Mwanza abwaga manyanga

Aliyekuwa Katibu wa Chadema Mkoa wa Mwanza, John Nzwalile (Kulia). Picha na mtandao

Muktasari:

Mbali na ukatibu wa mkoa, Nzwalile alikuwa mjumbe wa Baraza Kuu Taifa na mjumbe wa mkutano mkuu wa chama hicho taifa.

Mwanza. Katibu wa Chadema Mkoa wa Mwanza, John Nzwalile amejivua nyazifa zake tatu pamoja na uanachama wa chama hicho kwa madai kuwa chama hicho kimekuwa na ubabaishaji.

Mbali na ukatibu wa mkoa, Nzwalile alikuwa mjumbe wa Baraza Kuu Taifa na mjumbe wa mkutano mkuu wa chama hicho taifa.

Akizungumza na waandishi wa habari leo mkoani Mwanza, Nzwalile amesema Chadema kimekuwa kikiwachonganisha wananchi na Serikali, jambo ambalo amesema halikubaliki.

“Nimefikia uamuzi huu mgumu wa kujivua nyadhifa zangu zote na uanachama wa Chadema baada ya kuchoshwa na siasa za uchochezi, majungu na uchonganishi zinazofanywa na chama hiki kikubwa cha upinzani nchini,” amesema Nzwalile

Amesema imefika hatua viongozi wa Chadema wakijifungia ndani kwenye vikao vyake vinahusu maandamano na uchochezi pekee, kwanini “tusifanye shughuli za maendeleo badala ya kuhamasiha vurugu na uvunjifu wa amani,” amehoji Nzwalile.