Kauli ya JPM yazua mjadala mzito

Rais John Magufuli akihutubia wakati wa uzinduzi wa Mwaka Mpya wa kimahakama uliofanyika jijini Dar es Salaam juzi. Kutoka kulia ni Kaimu Jaji, Profesa Ibrahim Juma, Waziri wa Sheria na Katiba, Dk Harrison Mwakyembe na Jaji Mkuu wa Zanzibar, Omar Othman Makungu. Picha na Anthony Siame

Dar es Salaam. Kauli ya Rais John Magufuli kuhusu watu wanaowatetea wahalifu na kuwa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS) kimeingiliwa na siasa, imeibua mjadala mzito miongoni mwa wanasheria, baadhi wakisisitiza umuhimu wa sheria kufuatwa huku mwingine akisema mkuu huyo wa nchi hakuwa amemaanisha.

 Rais Magufuli aliwaonya wanaotetea wahalifu kwa mambo yaliyo wazi na kutaka nao wakamatwe na kuunganishwa kwenye kesi.

Rais Magufuli pia aliionya TLS akisema imeingiliwa na siasa na kwamba kuna chama ambacho hakukitaja kwa jina, akisema kinataka kuweka mtu wa kumpindua kiongozi wa chama hicho.

Alipotakiwa kuzungumzia kauli hizo jana, Rais wa TLS, John Seka alisema Rais alikuwa akifurahisha tu baraza lakini hakumaanisha.

“Kwa wale waliokuwa pale walimsikia vizuri Rais Magufuli, hata mimi nilikuwapo. Kauli ile ilikuwa ni ‘by the way’ tu hakumaanisha. Kwa mtazamo wake ni kwamba taasisi zinazosimamia haki zinapaswa kuwa na uzalendo, lakini sidhani kama alimaanisha. Alikuwa anafurahisha tu baraza,” alisema Seka.

“Mawakili wanaongozwa na sheria na Katiba, kama kuna wakili amekamatwa akiwa anatetea wateja wake sisi kama chama tutamtetea na tutatoa tamko. Inategemea sasa wakili amekamatwaje, wengine ni viongozi wa vyama vya siasa, inategemea umevaa muktadha gani,” aliongeza Seka.

Pamoja na maelezo hayo ya Seka, Wakili Peter Kibatala alisema anasubiri tamko la TLS kwani ndicho chama kinachosimamia ustawi wa mawakili. Alisema kabla ya kauli hiyo ya Rais, tayari kuna mawakili waliokamatwa wakiwa kazini.

“Tumeshuhudia mawakili watatu wakikamatwa wakiwa kazini. Mmoja alikamatwa kule Arusha lakini aliachiliwa baada ya mawakili wa TLS kumtetea kisheria. Mwingine ni Lawrence Masha ambaye alikamatwa mwishoni mwa mwaka 2015 alipokwenda kuwatetea wateja wake Kituo cha Polisi Oysterbay akidaiwa kuwatukana polisi,” alidai Kibatala.

“Mwingine alikamatwa kituo cha Polisi Magomeni alipokwenda kutetea wateja wake. Hayo yote yamefanyika kabla ya kauli hii ya Rais. Tunatarajia TLS watatoa tamko lisilo la kumung’unya.”

Akifafanua zaidi, Kibatala alisema kazi ya mawakili ni kuisaidia mahakama kupata ukweli na kuamua kwa haki.

“Huwezi kusema mtu ni mhalifu mpaka mahakama ithibitishe, hiyo ni haki ya kikatiba na ndiyo maana mawakili hawatetei watu walioko magerezani,” alisema na kuongeza:

“Mwalimu Julius Nyerere aliposhtakiwa na wakoloni kwa kosa la uchochezi, mbona alikubaliwa kutetewa na wakili? Hivi asingetetewa, leo tungekuwa wapi? Kazi ya wakili siyo kugeuza nyeupe kuwa nyeusi, ni ofisa wa mahakama,” alisema.

Wakili maarufu nchini, Felix Kibodya alisema mawakili ni maofisa wa mahakama ambao wanaisaidia kutenda haki.

“Kimsingi Wakili ni ofisa wa mahakama na kila raia wa Tanzania ana haki ya kutetewa na wakili. Hiyo ni haki ya kikatiba na Rais hayuko juu ya Katiba,” alisema Kibodya.

Hata hivyo, alikiri kuwapo kwa baadhi ya mawakili wasio waaminifu, wanaotetea wahalifu akisema huko ni kwenda kinyume cha kiapo cha uwakili.

“Mtu anakuja anakwambia ameiba Sh5 bilioni ila anataka umtetee. Hapo wakili unapaswa kumwambia ukweli kwamba hilo ni kosa na maelezo yake hayatatumika mahakamani bali ni siri ya wakili na mteja wake. Ukimtetea unakuwa unafanya uovu na ni kinyume cha kiapo cha uwakili,” alisema Kibodya.

“Kitu cha msingi ni ushahidi, wakili unasaidia kuweka wazi ukweli. Ni haki ya kikatiba na kimataifa siyo Tanzania tu,” aliongeza.

Mhadhiri wa Sheria wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Onesmo Kyauke aliwataka washauri wa Rais kumshauri vizuri kuhusu masuala ya kisheria kwa sababu kazi za uwakili ni za kikatiba.

“Wa kulaumiwa hapo ni washauri wake wa sheria, labda hawakumshauri vizuri kuhusu kazi za mawakili. Uwakili ni kazi ya kisheria na Katiba. Mtu akiwa polisi, anakuwa mtuhumiwa tu na anapaswa kupata dhamana na kutetewa na wakili,” alisema Dk Kyauke.

Wakili mwingine, Nyembea Stanslaus alirejea haki ya watu kusikilizwa kwa mujibu wa Katiba, akisema hiyo haiwezi kuondolewa na kauli ya Rais.

“Kila mtu ana haki ya kuchukuliwa kuwa hana hatia mpaka mahakama ithibitishe. Hiyo ni haki ya kikatiba na ndiyo maana wanampeleka mahakamani, vinginevyo wangemhukumu hukohuko,” alisema Nyembea.

Akizungumzia suala la siasa katika chama hicho, Seka alikanusha TLS kuhusishwa na misimamo ya vyama vya siasa.

“Hayo ni maoni yake binafsi, hiki ni chama kisichofungamana na chama chochote cha siasa, na ndiyo tunavitetea vyote bila kujali. Sijui kama kuna chama kinataka kuweka mtu wa kupambana nami, bado tuko kwenye mchakato wa uchaguzi, ila bado sijaamua kugombea,” alisema Seka.

Vuai amuunga mkono JPM

Licha ya Mbowe kukosoa kauli hiyo ya Rais Magufuli kuhusu mawakili, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai alisema anaiunga mkono.

Alisema kauli ya Rais Magufuli ililenga kuwataka mawakili kutenda haki na siyo kuwatisha katika kazi zao.

“Mimi namuunga mkono Rais, wala kauli yake haikulenga kuwatisha mawakili, bali anataka watende haki,” alisema Vuai.