Kauli ya Magufuli ya kuzaana yaibuka bungeni

Muktasari:

Mbunge aombo mwongozo kuhusu kauli hiyo

Dodoma. Mbunge wa Ndanda (Chadema), Cecil Mwambe amehoji kauli ya Rais John Magufuli ya kuwataka  watu kuzaa watoto kwa kadri wanavyoweza, akiitaka mifuko ya bima ya afya iongeze idadi ya watoto wanaowahudumia kutoka wanne hadi kufikia 10.

Mwambe akiomba mwongozo wa Spika bungeni leo, alisema uzazi wa mpango wanaufahamu na hata wanapokwenda katika bima ya afya idadi ya watoto wanaogharamikiwa na mfuko huo ni wanne.

“Kwa tafsiri yake kuna idadi ya inayotakiwa kuzaa kwenye familia na huduma inayotolewa. Serikali inatambua watoto wanne wanaweza kusaidiwa katika masuala ya bima na jana (juzi) tumemsikia mheshimiwa Rais akisema tuendelee kuzaa kadri tunavyoweza ‘as long as’ tunaweza kuwalisha na mengine,” alisema na kuongeza:

“Naomba mwongozo wako kwanini tunakuwa na Umati (Chama cha Uzazi na Malezi Bora Tanzania) ambacho kinasaidia masuala ya mpango wa uzazi? Basi tuongeze idadi ya watoto wanaoweza kutambulika rasmi kisheria kwasababu hao ndio tunaweza kuwazaa na kuwatunza.”

Mbunge huyo alishauri katika mfuko wa bima ya afya watu waruhusiwe kuingiza watoto 10 badala ya kuwekewa ukomo wa watoto wanne.

Akijibu mwongozo huo, Spika wa Bunge, Job Ndugai alisema huo ni ushauri.