Kaya 5457 kuondolewa kwenye mpango

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Utumishi na Utawala Bora  Angellah Kairuki amesema  jumla ya kaya 5457 zitaondolewa katika mpango wa kukomboa kaya masikini. Picha ya Maktaba

Muktasari:

  • Akizungumza mbele ya watendaji na wasimamizi wa halmashauri Kairuki alisema idadi hiyo imesababisha upotevu wa fedha nyingi ambazo hazikuwafikia walengwa wa mradi huo.

Dar es Salaam.Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Utumishi na Utawala Bora  Angellah Kairuki amesema  jumla ya kaya 5457 zitaondolewa katika mpango wa kukomboa kaya masikini kutokana na kutokuwa na sifa za kupata msaada huo.

Akizungumza mbele ya watendaji na wasimamizi wa halmashauri Kairuki alisema idadi hiyo imesababisha upotevu wa fedha nyingi ambazo hazikuwafikia walengwa wa mradi huo.

"Tutafanya ufuatiliaji wa karibu kwa wote waliohusika kuandikisha kaya zisizo na sifa na hakuna atakayeachwa  bila kuchukuliwa hatua za kisheria," alisema.

Aliongeza kuwa kaya hizo hewa hazitapewa fedha hizo kwa awamu ijayo ya nane   na badala yake kaya stahiki ambazo ni asilimia 76 zitaingia kwenye mpango huo.

Awali akisoma taarifa ya utekelezaji wa mradi huo Mratibu wa Mkoa TASAF Esterine Sephania alisema alisema licha ya kuwepo kwa changamoto kadha wa kadha mradi huo umesaidia kubadili hali za uchumi wa kaya masikini.

"Kaya zinaweza kupata mlo zaidi ya mmoja kwa siku na kuweza kufanya biashara ndogondogo" alisema.