Kenyatta akubali kukutana na Nasa

Muktasari:

Amesema atakuwa tayari kufanya hivyo iwapo mazungumzo yao yatakuwa na lengo la kuikwamua Kenya na wala siyo kujadili siasa

Nairobi, Kenya. Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta amesema yuko tayari kukutana na wapinzani kutoka muungano wa Nasa lakini akasema atakuwa tayari kufanya hivyo iwapo mazungumzo yao yatakuwa na lengo la kuikwamua Kenya na wala siyo kujadili siasa.

"Niko tayari kwa mazungumzo na yeyote," alisema Rais Kenyatta wakati akizungumza katika kongamano la magavana ambapo aliahidi kushirikiana nao kuimarisha Kenya.

Kongamano hilo liliandaliwa ili kutoa mafunzo kwa magavana wapya, ikiwa ni pamoja na kuchagua mwenyekiti mpya wa baraza la magavana.

Gavana wa Turkana, Josphat Nanok ndiye mwenyekiti wa baraza hilo kwa sasa na atatetea kiti chake kinachomezewa mate pia na Gavana wa Kwale, Salim Mvurya. Gavana wa Kirinyaga, Anne Waiguru anamezea mate kuwa naibu mwenyekiti wa baraza hilo.

Katika hotuba yake Rais Kenyatta alisisitiza kuwa mazungumzo anayotaka na Nasa ni ya kuendeleza taifa na siyo kujadili kuhusu siasa. Awali, alisema siasa zitajadiliwa mwaka 2022 ambapo Naibu Rais William Ruto anatarajiwa kupeperusha bendera ya  Jubilee (JP) kuwania kiti cha urais.

Rais Kenyatta hata hivyo, alisema sheria zilizomo kwenye katiba sharti zifuatwe katika kila hatua kufanya mazungumzo na kuendesha taifa mbele.

"Kila tunachofanya kiegemee kwa msingi wa katiba. Watakaofanya nje ya katiba na sheria za nchi watakabiliwa vilivyo," alionya kiongozi huyo.

"Serikali yangu haitaruhusu yeyote atakayecheza na kuhatarisha maisha ya Mkenya ama kuharibu mali yake. Hiyo laini ukipita, sheria ni sheria itachukua mkondo wake," alisema.

Aliahidi kufanya kazi na kila gavana licha ya mrengo wa kisiasa anaoegemea. Jumapili iliyopita kinara mwenza wa Nasa, Musalia Mudavadi alisema muungano huo unaomba kufanya mazungumzo na Serikali ya Jubilee ili kujadili uwezekano wa kuandaliwa kwa uchaguzi mwingine.

Aliyekuwa waziri mkuu, Raila Odinga hivi karibuni aliahirisha mipango yake ya kuapishwa kama wa wananchi na kusema kazi hiyo itafanyika baadaye bila kutaja tarehe.