Kesi mauaji ya dada wa bilionea Msuya yasomwa

Dada wa bilionea Erasto Msuya, Aneth Msuya wakati wa uhai wake

Muktasari:

Wakili wa Serikali, Diana Lukondo  alidai mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Margareth Bankika  kuwa Mei 25, 2016 katika eneo la Kibada, Kigamboni jijini Dar es Salaam, mshtakiwa huyo alimuua Aneth.

Dar es Salaam. Miriam Stephen Mrita (41) amefikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, akikabiliwa na shtaka la mauaji ya dada wa bilionea Erasto Msuya, Aneth Msuya.

Wakili wa Serikali, Diana Lukondo  alidai mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Margareth Bankika  kuwa Mei 25, 2016 katika eneo la Kibada, Kigamboni jijini Dar es Salaam, mshtakiwa huyo alimuua Aneth.

Baada ya kusomewa shtaka hilo, Miriam hakuruhusiwa kujibu chochote kwa sababu mahakama hiyo haina uwezo wa kusikiliza kesi za mauaji.

Upande wa mashtaka ulidai kuwa  upelelezi wa  kesi hiyo haujakamilika na iliahirishwa hadi Septemba 6. Mshitakiwa alirudishwa rumande kwakuwa kesi hiyo haina dhamana.

Aneth, ambaye ni dada wa bilionea Erasto Msuya, aliuawa kwa kuchinjwa na watu wasiojulikana Mei 25, 2016  nyumbani kwake Kibada, Kigamboni jijini Dar es Salaam.