Ugonjwa wa kichaa cha mbwa watajwa kuingia Moshi

Muktasari:

Amesema wamepokea taarifa kuwa katika hospitali ya Mtakatifu Joseph kuna wagonjwa wanne ambao wameng'atwa na mbwa na wanaendelea na matibabu.


Moshi. Ugonjwa wa Kichaa cha Mbwa umeripotiwa kuingia katika Manispaa ya Moshi Mkoa wa Kilimanjaro baada ya kuwepo kwa watu zaidi ya wanne waliong’atwa na mbwa na kulazwa hospitali.

Akizungumza leo Jumanne Machi 20, 2018 Mkurugenzi wa Manispaa ya Moshi Michael Mwandezi amesema wamepokea taarifa za kuwepo kwa ugonjwa huo na kuanza kuchukua tahadhari.

Amesema wamepokea taarifa kuwa katika hospitali ya Mtakatifu Joseph kuna wagonjwa wanne ambao wameng'atwa na mbwa na wanaendelea na matibabu.

Amebainisha kuwa kutokana na tatizo hilo tayari wanepokea maelekezo kutoka ofisi ya mkoa huo ya kuwataka kuchukua tahadhari.

Amesema kuna mbwa ambao wanazurura hovyo  na kung'ata watu, kwamba wameanza operesheni ya kuwaua mbwa wote ambao wataonekana wakizurura mitaani.

Alisema wameanza operesheni ya kuwaua mbwa katika Kata ya Kiboriloni na Mfumuni na watapita maeneo yote ya manispaa hiyo kuhakikisha  hakuna mbwa mitaani.

Aliwataka pia wananchi ambao watang'atwa na mbwa kuhakikisha wanafika kwenye vituo vya afya haraka ili kupata matibabu.

Mganga Mkuu wa Manispaa ya Moshi, Dk Somoka Mwakapalala amesema tayari wamepokea taarifa za watu wawili kung'atwa na mbwa katika kata ya Pasua na wanaendelea na Matibabu.

Amesema katika mwaka 2016 watu 434 waling'atwa na mbwa, 2017 watu 564 na kwamba kuanzia Januari hadi Februari 2018, watu 91 wameng’atwa.