Kikosi kazi cha watu 10 kuijenga upya Dodoma

Muktasari:

Ametoa kauli hiyo leo mchana (Jumamosi, Oktoba 1, 2016) wakati akizungumza na watumishi wa Serikali wa mkoa wa Dodoma, wazee wa mkoa huo, wafanyabiashara pamoja na viongozi mbalimbali kwenye ukumbi wa mikutano wa Dodoma (Dodoma Convention Centre).

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali imeunda timu ya wataalamu ambao watatoa ushauri juu ya suala zima la kuhamishia makao makuu Dodoma.

Ametoa kauli hiyo leo mchana (Jumamosi, Oktoba 1, 2016) wakati akizungumza na watumishi wa Serikali wa mkoa wa Dodoma, wazee wa mkoa huo, wafanyabiashara pamoja na viongozi mbalimbali kwenye ukumbi wa mikutano wa Dodoma (Dodoma Convention Centre).

Bila kutaja majina ya wajumbe wa timu hiyo, Waziri Mkuu amesema timu hiyo itaongezewa wataalamu kutoka China na Malaysia ambao nchi zao tayari zina uzoefu wa kuhamisha makao makuu ya nchi zao zaidi ya mara moja.

“Tumeunda timu ya watu 10 ambao ni wataalamu waliobobea kwenye masuala ya ujenzi wa miji mikuu, hawa wana uzoefu wa kuangalia makao Makuu ya nchi yanafananaje. Watakuja Dodoma, wapitie master plan na kisha watapita kwenye maeneo kadhaa ya mji ili waone hali halisi ikoje ndipo watupe maoni yao,” amesema.

“Tunataka tusirudie kosa la Jiji la Dar es Salaam la kulazimika kubomoa makazi ya watu kila inapolazimu kufanya uboreshaji wa miundombinu. Hawa watu watatuambia wapi tunatakiwa tuweke njia nne au sita za magari, wapi tuweke bustani au wapi tujenge nyumba za ghorofa moja, mbili, tatu au zaidi,” ameongeza.

Akifafanua kuhusu miundombinu, Waziri Mkuu amesema timu hiyo pia itatakiwa kutoa ushauri juu ya wapi ijengwe njia ya malori tu au mahali gani zinahitajika kujengwa barabara za juu (flyovers) ili kuepusha msongamano katikati ya mji wa Dodoma.