Kikwete amfariji Dk Mwakyembe

Muktasari:

Rais Kikwete amesema anafahamu kwamba Dk Mwakyembe ana majonzi lakini amemtaka awe mvumilivu katika kipindi hiki kigumu.

Dar es Salaam. Rais wa Serikali ya Awamu ya Nne, Jakaya Kikwete ni miongoni mwa waombolezaji wa kifo cha Linah, mke wa Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Dk Harrison Mwakyembe kilichotokea juzi.

Kikwete amewasili msibani leo, Julai 17 saa sita mchana na kuweka saini kwenye kitabu cha maombolezo.

Kikwete amemfariji Dk Mwakyembe na kumtaka awe mvumilivu katika kipindi hiki kigumu.

"Mwakyembe ni rafiki yangu wa siku nyingi, hata wakati mama anaumwa aliniambia na nilienda kumjulia hali alipokuwa Muhimbili, nimtake awe mvumilivu tunajua ana majonzi msiba huu ni wetu sote," amesema.

Wengine waliofika kumfariji Dk Mwakyembe ni Jaji Mstaafu Damian Lubuva, ambaye pia alimjulia hali Linah wakati akiwa hospitali.

"Mwezi uliopita nilienda Aga Khan kumuona mgonjwa mwingine lakini nikakutana na Mwakyembe, akaniambia mkewe amelazwa nikaona si vibaya kwenda kumjulia hali na alikuwa anaonyesha matumaini," amesema.

Wengine waliofika kumfariji Dk Mwakyembe ni Spika wa Bunge mstaafu, Anne Makinda; Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Ashatu Kijaji; Waziri wa Ulinzi, Dk Hussein Mwinyi; Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Biswalo Mganga na viongozi wengine wa Serikali waliopo madarakani na wastaafu.

Mjumbe wa kamati ya mazishi, Andrew Magombano amesema mwili wa Linah utaagwa kesho baada ya ibada itakayofanyika kwenye Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Usharika wa Kunduchi kuanzia saa nne asubuhi.

"Baada ya ibada tutaaga na saa saba kamili tutaelekea uwanja wa ndege tayari kwa safari ya kwenda Mbeya," amesema Magombano.