Kabila ataka sheria ya kulinda marais wastaafu

Muktasari:

  • Spika wa Bunge Aubin Minaku amesema, Rais Kabila amewataka wabunge wakutane kujadili na kupitisha sheria hiyo haraka iwezekanavyo.

Kinshasa, DR Congo. Wabunge wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, wanatarajiwa, kwa ombi maalumu la Rais Joseph Kabila, kukutana kwa lengo la kutunga sheria ya kuwalinda marais wanaostaafu.
Spika wa Bunge, Aubin Minaku amesema, Rais Kabila amewataka wabunge wakutane na kujadili na kupitisha sheria hiyo haraka iwezekanavyo.
Tangazo hilo linaweza kuwa ni ishara nyingine kwamba kweli Kabila anakusudia kung’atuka madarakani baada ya uchaguzi mkuu Desemba licha ya fununu kwamba anajaribu kufanya ghiliba ili akwepe kifungu kinachomzuia kugombea tena.
Waziri Mkuu Bruno Tshibala aliliambia shirika la Reuters wiki iliyopita kwamba Rais Kabila hatajitokeza tena kuwania urais likiwa ni tangazo la wazi zaidi kutoka kwa ofisa wa ngazi ya juu serikalini kuhusu suala hilo.
Lakini Kabila mwenyewe hajaweka wazi hadharani ikiwa hatagombea tena na baadhi ya wafuasi wake katika wiki za hivi karibuni walijenga uhalali wa kisheria ambao utamruhusu kugombea tena.
“Kutokana na ombi la rais wa jamhuri, kitaitishwa kikao maalumu cha Bunge,” alisema spika wa Bunge la Chini, Aubin Minaku alipozungumza na wasaidizi wake Ijumaa.
“Tutapitia mambo kadhaa yakiwemo kuangalia sheria kuhusu hadhi ya viongozi wa zamani, uteuzi wa mjumbe mpya katika mahakama ya katiba na sheria ya kodi ili kukuza sekta ya viwanda,” alisema.